skip to Main Content

DAR ES SALAAM

Ripoti ya Utafiti wa Afya, Viashiria na Malaria wa mwaka 2022 uliofanywa na Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) umeonyesha wanawake walioolewa wa mikoa ya Njombe, Kilimanjaro na Mbeya wanaongoza kutumia njia za uzazi wa mpango.

Mkoa wa Njombe unaongoza kwa matumizi ya njia hizo kwa asilimia 64, ukifuatiwa na Kilimanjaro (asilimia 63) na Mbeya (asilimia 58), takwimu hizi ni sawa na wastani wa wanawake watatu kati ya watano walioolewa katika mikoa hiyo wanatumia njia za uzazi wa mpango.

Aidha, katika ngazi ya Taifa, takwimu zinaonyesha wanawake walioolewa wanaotumia njia za uzazi wa mpango ni asilimia 38 huku kati yao asilimia 31 wanatumia njia za kisasa na asilimia saba bado wanatumia njia za asili.

Pia, takwimu hizo zinaonyesha wanawake wengi walioolewa wanatumia vipandikizi (asilimia 14) vikifuatiwa na sindano (asilimia tisa) kama njia za uzazi wa mpango.

Wakati wanawake walioolewa wakiendelea kutumia njia hizo za kupanga uzazi ndani ya ndoa pia, ripoti hiyo inaonyesha wanawake nchini wamepunguza uwezo wa kuzaa watoto kwa kipindi cha miaka 24.

Ripoti hiyo ya mwaka 2022 ilizinduliwa jijini Dodoma Januari 2023 na Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu ikiwa ni ya saba tangu ianze kutolewa ambapo ripoti ya kwanza ilitolewa mwaka 1999 ikionyesha hali ya Afya, Malaria na Ukimwi nchini.

Back To Top